Moroco yazindua kampeni ya maandalizi ya kombe la Dunia2026

Taifa hilo la Afrika kaskazini ambalo limewasilisha ombi lake la tano kuandaa fainali hizo , linakabiliwa na ushindani mkali kutoka ombi la pamoja linaloshirikisha Canada, Mexico na Marekani.
Mwenyekiti wa ombi hilo Moulay hafid Elalamy amesema kuwa Morocco itaonyesha mchezo mzuri zaidi, katika kombe hilo la dunia.
Uamuzi wa ni nani atakayeandaa kombe hilo utafanywa tarehe 13 Juni , mkesha wa kombe la dunia la mwaka 2018 mjini Moscow.
''Tunaahidi kuonyesha mchuano mzuri na kusheherekea thamani ya Umoja na amani'', aliongezea Elalamy.
''Maandalizi ya kombe la dunia nchini Morocco yataleta ufanisi wa kibiashara na kuwacha historia kubwa, na iwapo tutashinda heshima ya kuandaa dimba hilo tunaamini kwamba mshindi atakuwa soka, vijana wa taifa letu ,Afrika na dunia nzima kwa jumla''.
Hakuna maelezo yaliotolewa kuhusu miji andalizi huku kura ya kubaini atakayeandaa ikiwa umbali wa miezi mitano.
Taifa hilo la Afrika kaskazini limefeli katika maombi yake manne miaka 1994, 1998, 2006 na 2010.
Mwaka wa 2010, mchuano huo uliandaliwa na Afrika Kusini huku bara hili likiandaa kombe hilo kwa mara ya kwanza katika historia.
Morocco inataka kubadili hayo yote na imemteua Elalamy, waziri wa serikali, kuongoza ombi hilo huku aliyekuwa katibu mkuu wa shirikisho la soka Afrika Hicham El Amrani akiwa afisa mkuu mtendaji.

No comments